UJENZI WA MABANDA BORA YA SUNGURA



Hiki ni kizimba bora ambacho kinaonyesha kwamba juu kuna kizimba cha kuishi na chini ni kwa ajili ya sungura kucheza. 
Na Daniel Mbega
MPENDWA mjasiriamali, utakumbuka kwamba katika mfululizo wa makala hizi za ufugaji wa sungurakibiashara tumejifunza mambo mbalimbali ikiwemo uanzishwaji wa biashara hiyo ya mifugo, faida zitokanazo na ufugaji huo pamoja na aina mbalimbali zasungura wanaofaa kufugwa kwa matumizi mbalimbali.
Katika makala haya, tunaangalia namna ya ujenzi wa mabanda bora ya sungura ili wakuletee faida katika kipindi ambacho kuna mahitaji makubwa ya nyama.

Huku tukiangazia Dira ya Maendeleo ya Taifa ya 2025 ambayo inataka Watanzania wawe katika uchumi wa kati, pamoja na kuzingatia Maendeleo Endelevu ya Dunia yanayotaka kukomeshwa kwa umaskini pamoja na kuongeza upatikanaji wa chakula, biashara ya ufugaji wa sungura ni muhimu kuizingatia.
Najua faida ya mifugo kwa sababu nimezaliwa na kukulia katika mazingira ya ufugaji ingawa wakati huo hakukuwa na maendeleo kama ya sasa.
Leo hii ninapozungumzia fugaji wa sungura natambua kwamba uwekezaji huo unaweza kukuletea tija katika njia nyingi tu kama kuuza mkojo wa sungura kwenye maabara mbalimbali, kupata samadi kutokana na kinyesi chao ambacho pia hutumika kuzalishia mionyoo. Nyama, hata hivyo, ndiyo bidhaa kubwa na muhimu.
Ninachotaka kuwaelekeza hapa wajasiriamali wenzangu ni kitu rahisi tu katika uanzishaji wa ufugaji wa sungura kwa kuanzia na kile ulichonacho, siyo kama wanavyoelekeza wale wanaoitwa wataalamu.
Tunafahamu hali zetu za uchumi zilivyo, hivyo tukianza kuwaza kuhusu mtaji mkubwa kamwe hatuwezi kufanikiwa kwenye ujasiriamali.
Kwa maana hiyo, tunapaswa kuanza katika mazingira tuliyopo, kwa rasilimali zilizopo na tunaweza kukua taratibu hadi kufikia kwenye uwekezaji mkubwa katika ufugaji wa sungura.
Nitajaribu kueleza hatua kwa hatua tangu unapoanza ufugaji kwa mara ya kwanza na kueleza ni kwa vipi unaweza kukabiliana na changamoto ambazo hazijaandikwa kwenye vitabu au miongozo mingine. Lakini daima kumbuka kwamba, uzoefu ni mwalimu mzuri katika ujasiriamali.

Mambo ya msingi

Kuna mambo mengi ambayo unapaswa kuyafahamu kabla ya kuanza ufugaji wa sungura. Lakini nitajaribu kueleza kwa nia ya kukupa mwangaza wa namna ya kuanzisha ufugaji huo.
Kadiri unavyoendelea, na ikiwezekana, unatakiwa kupata taarifa za kutosha kuhusu ufugaji huo, kuanzia ujenzi wa mabanda, jinsi ya kuwahudumia, uchunaji wake baada ya kuwachinja, kuweka kumbukumbu na kadhalika.
Binafsi naweza kutumia dakika tano tu kumchuna sungura, tofauti na unavyotumia muda mrefu kunyonyoa kuku.
Sungura hawana msimu wa kuwafuga, unaweza kuanza ufugaji wakati wowote na wanaweza kuanza kuzaliana wakati wowote, tofauti na wanyama wengine.
Sungura majike wawili na dume moja wanaweza kukupatia wewe na familia yako kiasi cha kilogramu 81 za nyama kwa mwaka, kiasi ambacho ni kingi kwa familia za wastani wa watu watano.

Ujenzi wa Banda

 
 
Ufugaji wa sungura unaweza kufanywa mahali popote. Wafugaji wengi wanatumia mabanda, maeneo ya nyuma ya nyumba au kwenye maghala yasiyotumika kama mahali sahihi pa kuweka vizimba vya sungura.
Kumbuka: vizimba hivi ni sawa na vile vinavyotumiwa katika ufugaji wa kuku ingawa hivi vya sungura vinakuwa vipana na kimo kikubwa.
Unaweza kujenga banda kubwa la kawaida kwa kutumia miti inayopatikana kwenye eneo lako, mabanzi au mbao, ambazo pia zinapatikana.
Ikiwezekana, unaweza kujenga ukuta wa matofali na kuacha madirisha na kuziba kwa nyavu nene pamoja na nyavu ndogo (kama za mbu) ili kuzuia wadudu wasiingie. Kumbuka kwamba, sungura wanahitaji kupata hewa ya kutosha, lakini pia wanapenda sehemu zenye kiza kidogo. Banda hilo lazima liezekwe vizuri ili lisivuje hasa nyakati za masika.
Ukubwa wa banda ambalo unaweza kulitumia kuweka vizimba vya sungura linategemea na idadi ya sungura unaotaka kuwafuga. Wale wa kuanzia hawana shida, lakini nazungumza kuhusu malengo ya mradi wako.
Unaweza kujenga banda lenye upana wa futi 16 na urefu wa futi 24. Kimo cha paa la katikati ni lazima kiwe futi 12 kuanzia kwenye sakafu na pembeni ni lazima liwe na kimo cha futi 8.
Gharama za ujenzi wa banda la aina hiyo zitategemea na rasilimali ulizotumia kujengea.
Kama unafuga kibiashara, weka sakafu nzuri kwa sababu utatumia njia bora za kukinga mkojo ambao ni mali. Lakini kama hutaki kukinga mkojo, basi usisakafie ili mkojo ukidondoka uweze kuzama ardhini na inakusaidia katika kusafisha na kuondoa harufu. Sakafu imara ya kawaida inakupasa usafishe kila wakati, hasa kama hukutumia njia bora za kukinga mkojo.
Lakini nakushauri, kinga mkojo kwa sababu ni mali. Utapata fedha nyingi bila kutegemea.
Vizimba ambavyo vimeinuliwa na kutengeneza bati maalumu kwa ajili ya kukikanga mkojo.
Kama hutaki kutumia vizimba, kamwe usiwaweke sungura wako kwenye sakafu ya udongo, kwa sababu sungura wana kawaida ya kuchimba na unaweza kukuta wametoboa ardhi na kutoka nje.
Sakafu ya udongo itakufanya upate shida pia wakati sungura wanapozaa, kwani wanaweza kuzalia kwenye mashimo.
Hivyo basi, kama utawafuga bila kutumia vizimba, weka sakafu na uweke matandazo sakafuni.

Vizimba
Vizimba (hutches au cages) lazima vitengenezwe kabla ya kuwaingiza sungura wako wa kwanza. Sungura mmoja anapaswa kuwa na nafasi ya upana wa futi mbili, urefu wa futi tatu na kimo cha futi tatu – pamoja na eneo la kutosha la kuchezea.
Unaweza kujenga vizimba vikubwa kuwezesha kuweka sungura wengi ambao unapanga kuwalisha tu kwa ajili ya kuwauza kwa nyama. Kwa kadiri kizimba hicho kitakavyokuwa, ni vyema kukiinua kutoka usawa wa ardhi ili kukusaidia kuondoa takataka unapofanya usafi.

Eneo la kuishi – wastani wa 12 sq. ft (6 x 2) ambalo linaweza kuwa na sungura wadogo na wa maumbile ya kati wanne. Ikiwa sungura wako ni wa aina ya wale wakubwa, basi unatakiwa kuongeza ukubwa wa banda.

Eneo la kuishi la sungura wako kwenye kizimba ni lazima lihusishe eneo la kulala, eneo la kudondoshea kinyesi na vifaa vya chakula na maji na nafasi ya kutosha ya kuweza kucheza. Ni vyema sungura wako wakawa na eneo la kutosha kujinyoosha katika kila upande. Eneo la kuishi la sungura wako likiwa dogo litaathiri afya yake – na kumsababishia matatizo ya uti wa mgongo, kupoteza nyama na utapiamlo.

 

Upana wa kizimba

Sungura aliye huru lazima atajinyoosha anapokuwa amepumzika, hivyo kizimba chako kinatakiwa kiwe kipana kuwezesha sungura alale huku akiwa amenyoosha miguu yake yote. Hii inatoa nafasi ya kutosha kuweza kujigeuza.
Wastani wa upana unatakiwa kuwa futi 2 (60sm) kwa sungura wadogo na wa kati na futi 3 (90sm) kwa sungura wakubwa kama wa aina ya Flemish Giants.

 

Urefu wa kizimba

Kizimba kinapaswa kuwa kirefu kidogo ili kumwezesha aruke mara tatu hadi mara nne bila kuigonga pua yake mwisho wa kizimba. Sungura wa umbile la kati anaruka kwa umbali wa inchi 18 (45sm) kwa kila mruko mmoja.
Kama upana wa kizimba chako ni futi 2, urefu unapaswa kuwa futi 6 ili kufanya jumla ya futi za eneo 12.

 

Kimo cha kizimba

Sungura husimama kwa miguu yao ya nyuma ili kuangalia kama mazingira yao ni salama, na kizimba chako lazima kiwe na urefu unaomruhusu kusimama bila kujigonga kichwani ama masikio yake kugusa juu ya dari.
Kimo cha futi 2' (60sm) mara nyingi kinafaa kwa sungura wa ukubwa wa kati lakini aina kubwa za sungura zinahitaji kimo cha futi 3' (90sm).

Eeneo la kuchezea – wastani 32 sq. ft.

Kiwango cha wastani kinachopendekezwa kwa ajili ya eneo la mazoezi ni eneo la futi 32 (mfano; futi 8'x4'). Kama ilivyo kwa eneo la kulala, sungura wako atahitaji eneo la kusimama wima. Ingawa siyo lazima, lakini husaidia sungura wako kuongeza urefu wakati wa kuruka.
Kama utaunganisha vipimo hivi kwa pamoja, kizimba chako kinapaswa kuwa na eneo la futi 48 (upana futi 6 x urefu futi 8).
Lakini eneo la kuchezea tu haitoshi, bali unatakiwa kuweka na vitu ambavyo sungura atachezea kama vipande vya vigogo ambako anaweza kupanda na kusimama, mabati unayoweza kuyakunja kama duara ndefu ambamo anaweza kupita kana kwamba anaingia kwenye shimo na kutokea upande wa pili, na kadhalika.

Eneo lako likiwa kubwa, hasa kama unawafuga kwa nje, yaani kama vizimba haviko ndani ya banda, unaweza kutengeneza eneo la kuchezea lilio bora zaidi.

Artikel Terkait